Tuesday, 10 September 2013

Hivi ndivyo tutakavyoinua elimu ya msingi na sekondari nchini

Hivi karibuni Serikali ilizindua mpango ujulikanao kwa jina la  ‘’Matokeo Makubwa Sasa’’, uliohusu sekta mbalimbali zenye changamoto zinazohitaji ufumbuzi wa haraka.
Sekta zilizoainishwa chini ya mpango huo ni elimu, miundombinu, madini na nishati, uchumi na fedha pamoja na sekta ya maji.
Katika sekta ya elimu, wataalamu kutoka ndani na nje ya vyombo vya Serikali vinavyoshughulikia elimu, walikutana na kuandaa mikakati tisa ya kunusuru sekta ya elimu nchini, hasa elimu ya msingi na ile ya sekondari.
Pamoja na mambo mengine, mikakati hiyo inalenga kwa kiwango kikubwa kuinua kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa  ngazi hizo muhimu katika mfumo wa elimu nchini.
Makala haya yanadurusu kwa kina maelezo ya mwongozo wa namna mikakati hiyo itakavyotekelezwa ndani ya kipindi cha miaka mitatu ya mpango.
Ujenzi wa miundombinu muhimu shuleni
Shughuli za ujenzi zilizobainishwa kutekelezwa katika mpango huu ni pamoja na ujenzi, ukarabati na  ukamilishaji majengo kama  madarasa, maabara, vyoo, utoaji wa maji safi na kuweka umeme kupitia gridi ya Taifa au umeme wa mwanga wa jua.
Serikali imepanga kuwezesha utekelezaji wa haraka wa mradi wa awamu ya pili ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES II) katika ujenzi wa miundombinu ya msingi kwa shule 1,200 ifikapo mwaka 2014.
Serikali imepanga kukamilisha ujenzi wa shule hizi katika awamu tatu: awamu ya kwanza itakamilika Septemba 2013 ambapo shule za sekondari 264 zitajengwa.
Awamu ya pili itakamilika Machi 2014 ambapo shule za sekondari 528 zitahusika na  awamu ya tatu itakamilika Septemba 2014 ambapo shule za sekondari 408 zitajengwa au kukarabatiwa.
Mgawanyo wa shule kimkoa katika awamu kwanza unahusisha Arusha (14), Dodoma (12), Dar es Salaam (6), Geita (6), Iringa (8), Kagera (14), Katavi (4), Kigoma (8), Kilimanjaro (14), Lindi (12), Manyara (12), Mara (12) Mbeya (16), Morogoro (12),  Mtwara(12), Mwanza (11), Njombe (8), Pwani (14), Rukwa (6) Ruvuma (10), Shinyanga (8), Simiyu (7), Singida (8), Tabora (12)  na Tanga (18).
Ruzuku ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia:
Katika kutekeleza mpango, Serikali inatoa ruzuku ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia  kwa kuzipa shule uwezo wa kununua vitabu na vifaa vingine na kuimarisha usimamizi na uendeshaji wa shule.
Kiwango cha ruzuku kilicholengwa kwa mwaka ni Sh 25,000 kwa kila mwanafunzi wa elimu ya sekondari na shilingi 10,000 kwa mwanafunzi wa elimu ya msingi.
Aidha, Serikali imepanga kuinua ufaulu katika shule kwa kuboresha upatikanaji  wa vitabu vya kiada na vifaa vya kufundishia na kujifunzia shuleni, na kuhakikisha vifaa vya kufundishia na kujifunzia vinafika shuleni na kutumika.
Upangaji wa shule kuzingatia matokeo
Serikali imeanza kuzipanga shule kitaifa kwa kuzingatia matokeo, kwa lengo la kuongeza uwajibikaji na ushiriki wa jamii katika usimamizi wa utoaji wa elimu bora. Uwajibikaji ni kati ya changamoto kubwa zinazoukabili mfumo wa elimu kwa sasa.
Shule zitapangwa kwa ubora wa matokeo katika mitihani na kisha kutangazwa kwa umma, ili iwe chachu ya kuandaa jamii kuwajibika na kuleta uelewa mpana.
Faida za upangaji wa shule ni pamoja na kuziamsha shule kufanya vizuri, itasaidia shule kujitathmini, itawahamasisha walimu na wanafunzi kufanya kazi kwa bidii na kuzitambua shule zilizofanya vizuri zaidi.
Shule zitakazofanya vibaya zitafuatiliwa na kupewa msaada kulingana na upungufu uliojitokeza. Shule zitakazoonyesha maendeleo chanya kwa asilimia 10 ukilinganisha na mwaka uliopita zitapewa tuzo.
Utaratibu wa kutoa tuzo kwa shule utatoa motisha kwa shule kuongeza bidii na kutoa matokeo bora zaidi. Tuzo hii itaanzia katika matokeo ya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi na sekondari.
Aidha, tuzo za fedha taslimu na nyinginezo zitatolewa katika makundi mawili ya shule,  ambayo ni shule zilizoonyesha maendeleo ya juu na shule zilizofanya vizuri. Nafasi za ushindi zitagawanywa katika mikoa yote ili kupata msambao wa utoaji wa tuzo hizo.
Pia shule zitapanga utaratibu wa kugawana tuzo kwa uwazi na ushirikishwaji. Tuzo zitakazotolewa kuanzia mwaka huu zitajumuisha fedha, vyeti, vifaa mbalimbali, ngao na vikombe.
Motisha kwa walimu 

Katika kuboresha ufundishaji na ujifunzaji, Serikali imeandaa mkakati wa kuwatambua  walimu wanaofanya kazi  vizuri kwa kuwapa tuzo, kuhakikisha madeni yote ya walimu yanalipwa kwa wakati na kuandaa mpango wa motisha kwa walimu wanaofanya kazi katika maeneo yenye mazingira magumu.
Motisha kwa walimu ni muhimu kwa kuwa kazi ya ualimu ni kazi yenye  jukumu la kumwandaa Mtanzania atakayesheheni maarifa, ujuzi na stadi za kukabiliana na changamoto za kimaendeleo.
 Aidha, walimu wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo madai mbalimbali kutoshughulikiwa kwa , hali inayosababisha walimu wengi kukata tamaa.
Katika kutekeleza mkakati huu wa motisha kwa walimu, kuanzia Julai 2011 hadi sasa Serikali imelipa madai ya malimbikizo ya mishahara ya walimu 31,779 yenye thamani ya  Sh 28.5 bilioni, ambapo Sh 28,544,743,604.06 zimelipwa kupitia mishahara ya watumishi husika.
Pia kutoka  Januari 2012 hadi Juni, 2013, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imelipa madai yasiyo ya mishahara ya walimu 2,825 yenye jumla ya Sh.2.6 bilioni kati ya shilingi 3.3 bilioni ya fedha kutoka Hazina. Lakini pia Serikali kwa sasa inaendelea na majadiliano na Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kuhusu kuboresha zaidi maslahi ya walimu.
Kuwajengea uwezo walimu na wanafunzi
Programu ya kujenga uwezo wa walimu na wanafunzi katika ujifunzaji na ufundishaji imeanzishwa ili kutatua changamoto ya msongamano wa wanafunzi darasani ambao husababisha wanafunzi wenye kuhitaji msaada katika ujifunzaji kushindwa kusaidiwa.
 Pia kuna changamoto ya baadhi ya walimu kutokuwa na  nyenzo muhimu za kufundisha kwa ufanisi, kama vile kushindwa kuandaa maandalio ya somo na  kutokuwepo kwa utaratibu wa kuwasaidia wanafunzi katika maeneo yenye changamoto za uelewa kwa baadhi ya shule.
Katika kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika ufundishaji na ujifunzaji, Serikali itaendesha mitihani ya majaribio kwa ajili ya kuwabaini wanafunzi wenye mahitaji ya ziada katika kujifunza, kutoa mafunzo kwa walimu kwa ajili ya utekelezaji na kutoa mafunzo rekebishi kwa wanafunzi kwa kuzingatia maeneo yenye changamoto za kuelewa.
Programu hii inawalenga walimu wa masomo ya Bayolojia, Hisabati, Kiswahili na Kiingereza katika ngazi ya sekondari na walimu  Hisabati, Kiswahili na Kiingereza kutoka  shule za msingi. Walengwa wengine ni wanafunzi wa darasa la saba na kidato cha nne kuanzia mwaka 2013 hadi 2015.

No comments: