Saturday, 11 July 2015

Hongera Rais Kikwete, changamoto bado nyingi

Rais Jakaya Kikwete juzi alihutubia Bunge la 10 kwa lengo la kuliaga na kulivunja rasmi kuashiria kuweka mazingira kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu ambao utatoa Bunge la kumi na moja.
Rais alitumia hotuba yake ya mwisho kwa chombo hicho cha kutunga sheria kuelezea mafanikio ambayo Serikali ya Awamu ya Nne imeyapata katika kipindi cha miaka 10 ya uongozi wake, lakini pia akawa muwazi kwa kueleza matatizo ambayo hakuweza kuyafikia, hasa suala la bei ya mazao kwa wakulima na kushindwa kulifufua Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).
Tunaungana na Watanzania wengine kumpongeza Rais kwa jitihada ambazo Serikali yake imezifanya katika nyanja za uchumi, siasa na jamii na hatuna shaka na takwimu alizozitoa kuelezea mafanikio hayo.
Ni jambo lisilopingika kuwa alijitahidi kuimarisha utawala bora, hasa baada ya kuruhusu taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kuwasilishwa bungeni ambayo imesaidia kudhibiti ufisadi kwenye vyombo vya umma, kuendeleza ujenzi wa miundombinu ya usafiri-barabara, bandari na viwanja vya ndege- huduma za afya, ukusanyaji kodi, demokrasia na Muungano.
Kama alivyosema Rais, si rahisi kumaliza matatizo yote katika awamu moja na hivyo atakayempokea kijiti ana wajibu wa kuendeleza hayo atakayoyakuta hadi atakapoishia. Pamoja na kumpongea Rais kwa hotuba hiyo na mafanikio ya Serikali ya awamu yake, tunadhani kuna mambo ambayo hayakuwa na mafanikio makubwa au yalifanyiwa kazi vizuri lakini yanaanza kuonekana kwenda mrama.
Suala la Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK) ni moja ya mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Nne, lakini ni jambo linalosikitisha kwamba Rais Kikwete anaondoka wakati umoja huo ukiwa na dalili za kumomonyoka.
Matukio ya hivi karibuni kwenye Baraza la Wawakilishi ni ishara tosha kwamba mambo si shwari Zanzibar na hivyo badala ya Rais kusifia mafanikio, angechukulia kuwa ni changamoto kubwa kwa Serikali yake kushindwa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana.
Pia, suala la Muungano halionekani kuwa linaachwa salama kwa sababu kipindi hiki ndicho ambacho pande hizi mbili zimerushiana maneno makali yanayoweka ishara mbaya kwa mustakabali wa tunu hiyo muhimu kwa Taifa.
Ni dhahiri matukio yaliyojiri wakati wa Bunge la Katiba yanatosha kuweka swali juu ya hatima ya Muungano, hasa baada ya viongozi wa chombo hicho kushindwa kutafuta suluhu ili kuwa na maridhiano ambayo yangejenga mazingira mazuri kwa Taifa kusonga mbele likiwa kitu kimoja.
Pamoja na Rais kusema kuwa anaiacha nchi ikiwa salama, bado kuna maswali mengi kuhusu usalama huo, amani na utulivu. Ni kweli kwamba vitendo vya ujambazi vimepungua kulingana na hali ilivyokuwa mwaka 2005 wakati akiingia madarakani, lakini hali inaonekana si shwari kwa kuwa uhalifu huo sasa ni dhidi ya polisi na vituo vyao.
Uvamizi wa vituo vya polisi ambao jukumu lao ni kulinda usalama wa raia, sasa umekuwa ukitokea kila mara, tishio la ugaidi limeongezeka na vitendo vya wananchi kujichukulia sheria mkononi wanapokuwa na madai yao vimeongezeka. Mambo hayo, ukichanganya na ukweli kwamba takwimu zinazoashiria kukua kwa uchumi, hazionekani kwenye maisha ya kila siku ya mwananchi wa kawaida, yanazidi kuiweka amani yetu katika hali ya sintofahamu.
Tunadhani kuwa haya ni mambo ambayo inabidi yawekwe bayana ili Taifa lijue kuwa pamoja na mafanikio mengine mengi aliyoyataja mkuu wa nchi, bado tuna changamnoto hizo kubwa na hivyo hata Rais anayekuja na Serikali yake, anapaswa kujua kuwa nchi ina mzigo kiasi gani katika kudumisha Muungano, kuendeleza usalama wa raia na kulinda muafaka uliofikiwa Zanzibar.

No comments: