Utamaduni wa Mtanzania, katika sekta ya burudani, unaweza
ukapotea kama waongeaji tusipotumia majukwaa yetu ya kuongelea na
kuliongelea hili angalau kwa uchache.
Uchunguzi wa jarida hili umegundua hili na
nachukua wasaa huu kama mshikadau wa burudani hapa nchini kuwaambia
wandaaji, tuangalie upya aina za burudani tunazotoa na watu
tunaowapelekea.
Kiukweli tunaanguka na kwa kuanguka sisi
tutajikuta siku moja tukiangusha maadili ya kijana wa kitanzania pia na
burudani ni ajira kwa vijana wetu sasa tukisababisha itumike ndivyo
sivyo, kutakuwa na hatari ya kuliletea hasara taifa katika siku za
usoni.
...Nina maana yangu kusema hivi.
Katika miezi sita ya nyuma nimeshuhudia matamasha
mengi ambayo majina yake hayaendani na kinachofanyika kwenye tamasha
hilo, hali inayosababisha watu makini wa tasnia ya burudani kuanza
kushindwa kabisa kuwaelewa waandaaji, wamekuwa kama wadanganyifu hivi
sifa ambayo si nzuri kwa mfanyabiashara aliyedhamiria kukaa kwenye
tasnia kwa muda mrefu.
Tamasha linaitwa la kimataifa, lakini
kinachopatikana kwenye tamasha hilo utakuta ni kama tamasha la Dar es
Salaam hivi, sasa sijui ni kutokana na bajeti au ni kutokana na ufinyu
wa fikra ama ni kutokana na uroho wa kipato au ni kuhisi kwamba wale
unaowapelekea burudani hawana akili?
Unapomwambia mtu naleta kitu cha kimataifa, halafu zinaonekana sura za hapahapa unataka kusema kwamba sisi ni wa kimataifa?
...tangu lini?
Basi kuwe na angalau na uwakilishi wa nchi mbili tatu...
Hamna!
Tunamdanganya nani sasa?
Tunajidanganya wenyewe kwa taarifa maana mwisho wa
siku Watanzania si wajinga tena, wanajua mambo mazuri na mabaya,
..unaona bwana? Mwisho wa siku wakishajua wewe si mkweli kwenye kazi
zako watakukimbia na wakikukimbia utataka kumtafuta mchawi, kumbe
umejiloga mwenyewe.
Kuna haja ya kuwa makini katika hili ndugu zangu wadau, kuna
watu wana akili zao wamekaa tu wanaangalia haya mambo, wanachambua tu na
mwishowe watatoa hoja zao na unaweza kuhisi unaonewa, kumbe ndiyo
stahili yako.
Ukisema kitu ni cha kimataifa, kiwe cha kimataifa
kweli, kikiwa kitu cha kiasili kiwe cha kiasili kweli na wasanii jamani
wapo wengi, siyo kila siku wale wale tu tutoe nafasi kwa kizazi
kilichopo mtaani kuonyesha uwezo wake tusiangalie tu walio karibu yetu.

No comments:
Post a Comment