Saturday, 13 September 2014

Hii nayo ni sanaa ya kimataifa

Utamaduni wa Mtanzania, katika sekta ya burudani, unaweza ukapotea kama waongeaji tusipotumia majukwaa yetu ya kuongelea na kuliongelea hili angalau kwa uchache.
Uchunguzi wa jarida hili umegundua hili na nachukua wasaa huu kama mshikadau wa burudani hapa nchini kuwaambia wandaaji, tuangalie upya aina za burudani tunazotoa na watu tunaowapelekea.
Kiukweli tunaanguka na kwa kuanguka sisi tutajikuta siku moja tukiangusha maadili ya kijana wa kitanzania pia na burudani ni ajira kwa vijana wetu sasa tukisababisha itumike ndivyo sivyo, kutakuwa na hatari ya kuliletea hasara taifa katika siku za usoni.
...Nina maana yangu kusema hivi.
Katika miezi sita ya nyuma nimeshuhudia matamasha mengi ambayo majina yake hayaendani na kinachofanyika kwenye tamasha hilo, hali inayosababisha watu makini wa tasnia ya burudani kuanza kushindwa kabisa kuwaelewa waandaaji, wamekuwa kama wadanganyifu hivi sifa ambayo si nzuri kwa mfanyabiashara aliyedhamiria kukaa kwenye tasnia kwa muda mrefu.
Tamasha linaitwa la kimataifa, lakini kinachopatikana kwenye tamasha hilo utakuta ni kama tamasha la Dar es Salaam hivi, sasa sijui ni kutokana na bajeti au ni kutokana na ufinyu wa fikra ama ni kutokana na uroho wa kipato au ni kuhisi kwamba wale unaowapelekea burudani hawana akili?
Unapomwambia mtu naleta kitu cha kimataifa, halafu zinaonekana sura za hapahapa unataka kusema kwamba sisi ni wa kimataifa?
...tangu lini?
Basi kuwe na angalau na uwakilishi wa nchi mbili tatu...
Hamna!
Tunamdanganya nani sasa?
Tunajidanganya wenyewe kwa taarifa maana mwisho wa siku Watanzania si wajinga tena, wanajua mambo mazuri na mabaya, ..unaona bwana? Mwisho wa siku wakishajua wewe si mkweli kwenye kazi zako watakukimbia na wakikukimbia utataka kumtafuta mchawi, kumbe umejiloga mwenyewe.
Kuna haja ya kuwa makini katika hili ndugu zangu wadau, kuna watu wana akili zao wamekaa tu wanaangalia haya mambo, wanachambua tu na mwishowe watatoa hoja zao na unaweza kuhisi unaonewa, kumbe ndiyo stahili yako.
Ukisema kitu ni cha kimataifa, kiwe cha kimataifa kweli, kikiwa kitu cha kiasili kiwe cha kiasili kweli na wasanii jamani wapo wengi, siyo kila siku wale wale tu tutoe nafasi kwa kizazi kilichopo mtaani kuonyesha uwezo wake tusiangalie tu walio karibu yetu.

No comments: