Dodoma. Jina la mwanasiasa James Mbatia si
geni sana miongoni mwa Watanzania na amejizolea sifa ya kutanguliza
masilahi ya taifa tangu mchakato wa kupata Katiba Mpya ulivyoanza.
Mbatia, ambaye alishiriki katika harakati za
kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi miaka ya 1990, mara nyingi
amejitokeza kusaka mwafaka pale inapotokea sintofahamu kwenye vikao vya
Bunge Maalumu la Katiba.
Busara aliyoitumia wakati wa upitishaji wa muswada
wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka
2013, ndiyo aliyoirudia katika Bunge Maalumu la Katiba.
“Dalili za kutopatikana kwa Katiba Mpya zimeanza
kuonekana, ni vizuri ikatumika busara na hekima katika kuvuka kikwazo
hiki na njia pekee ni maridhiano,” alisema Mbatia, Septemba, mwaka
jana.
Mbatia aliyotoa maneno hayo baada ya wabunge wote
kutoka kambi ya upinzani isipokuwa Mwenyekiti wa TLP, Augustino Mrema wa
TLP kususia upitishaji wa muswada kupinga ubabe wa CCM.
“Sisi siyo tutakaoifanya Tanzania isitawalike bali
CCM. Tunafanya haya kwa nia njema kabisa hatutaki damu ya Watanzania
imwagike kwa jambo linaloepukika,” alisema Mbatia katika kipindi hicho.
Katika kipindi hiki cha Bunge la Katiba, busara
hiyo ndiyo imetumika ili kusawazisha mambo wakati yalipokuwa yanakwenda
vibaya kwenye semina ya kujadili Rasimu ya Kanuni.
Bunge hilo lilikuwa katika hati hati ya kuvunjika
katika siku za awali tu za utungaji wa Katiba pale lilipojikuta likiwa
njia panda kuhusu kuamua aina ya kura itumike kuamua vifungu vya Rasimu.
Kwanini Mbatia anaamini falsafa ya Katiba ni tendo la maridhiano?
Katika mahojiano maalumu na gazeti hili, Mbatia
anasema Katiba siku zote ni tendo la maridhiano na kutoa mfano wa
Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.
“Mwezi Aprili 22, mwaka 1964, Rais Nyerere
(Julius) alikaa na Rais Karume (Abeid) wa Zanzibar wakakubaliana kuwa
nchi hizi ziungane, hili lilikuwa tendo la maridhiano,” anasema Mbatia.
“Kwa hiyo Aprili 24, mwaka 1964 Bunge la
Tanganyika lilikaa na kutunga sheria ya maridhiano hayo na baadaye
Aprili 26, mwaka huo, Muungano ukazaa nchi inayoitwa Tanzania,” anasema
Mbatia.
Kwa msingi huo, Mbatia ambaye pia ni Mjumbe wa Bunge Maalumu la
Katiba, anasema siku zote maridhiano yanaanza kwanza na watu
wakishaafikiana ndio wanayatungia sheria.
“Tuna mfano mwingine wa kujifunza kule Zanzibar,
Seif Shariff Hamad (Katibu Mkuu CUF) na Rais Amani Karume walijifungia
Ikulu Novemba mwaka 2009 na wakafanya tendo la maridhiano,” anasema.
“Walikaa wao wawili tu wakaridhiana kuwa watafute
mwafaka na baada ya kuridhiana Baraza la Wawakilishi la Zanzibar,
likaitwa na kufanya mabadiliko ya 10 ya Katiba ili kuunda Serikali ya
Umoja wa Kitaifa,”anasema Mbatia.
Mbatia anasema maridhiano hayo ndiyo yaliyowafanya
Watanzania na watu wengi duniani washuhudie Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar
wa mwaka 2010 ukifanyika bila tone la damu ya Mzanzibari kumwagika.
“Tume ya Jaji Warioba (Joseph) imekusanya maoni ya
Wanzania na kupendekeza muundo wa Serikali tatu kuwa ndiyo chaguo la
Watanzania lakini leo CCM wanatilia shaka uadilifu wa Jaji Warioba.
“Nawashauri rafiki zangu wa CCM wasianze kuhoji
leo uadilifu wa Jaji Warioba. Yeye na mzee Butiku (Joseph) ni wafuasi wa
karibu sana wa Nyerere lakini wameheshimu maoni ya Watanzania,” anaonya
Mbatia.
Mbatia anasema ni vizuri wajumbe wa Bunge Maalumu
la Katiba, wakaiboresha Rasimu ya Katiba na kwamba kama kuna hoja mpya
za kujenga ziingizwe lakini si kwa vitisho na ubabe.
“Kulazimisha mambo yenye mwelekeo wa kupatikana
kwa Katiba yenye masilahi mapana ya CCM, litakuwa jambo la kutowatendea
haki Watanzania na hicho kitakuwa ndiyo chanzo cha machafuko,” anaeleza
Mbatia.
Mbatia anasema ni katika msingi huo huo wa kutaka
Tanzania isiingie kwenye machafuko, ndiyo maana alipendekeza kuundwa kwa
Kamati ya Maridhiano baada ya kujitokeza kwa dalili mbaya.
“Tulikuwa tumekwama katika njiapanda…CCM
wameng’ang’ania kura ya wazi wakati wanajua si matakwa ya kidemokrasia,
sasa mimi nikaona hapana hebu turudi kwenye maridhiano,” anasema Mbatia.
Mbatia anasema kwa moyo huo huo wa maridhiano
alioupendekeza, ndio ulisaidia kupatikana kwa mwafaka juu ya kanuni ya
37 na 38 ya Bunge Maalumu la Katiba na kuongeza;
“Bila kuundwa kwa kamati ya maridhiano nina hakika
Bunge hili lingekuwa limeshasambaratika lakini bado ‘spirit’ (moyo) ipo
na hali hii ndiyo tunataka iendelee kwa sababu bado tuna shughuli pevu.
Mbatia anasema kutaibuka mvutano katika vifungu hivyo pale
watakapofikia hatua ya kupitisha ibara za Katiba na kuwataka CCM wasome
alama za nyakati na kutazama matakwa ya Watanzania.
“CCM waelewe kuwa Watanzania wanatutazama, leo
wanapolazimisha kura ya wazi kupitisha Katiba halafu tukienda kwenye
kura ya maoni Katiba hiyo hiyo ipigiwe kura ya siri, hakuna
atakayewaelewa.”
Mbatia aliongeza kusema; ”Hakuna ubishi kuwa
mabadiliko ya 10 ya Zanzibar yalikiuka Katiba ya Muungano na Watanzania
wanalifahamu hilo lakini hoja ya msingi hapa ni maridhiano.”
Mabadiliko hayo ndio yaliyotamka kuwa Zanzibar ni
nchi yenye mipaka yake, ina Katiba yake, ina bendera yake na ina wimbo
wake wa Taifa, kitendo kinachotafsiriwa kuwa ni uhaini kwa mujibu wa
Katiba ya Muungano.
Mbatia ni nani hasa?
Mbatia ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania wa kuteuliwa na Rais, Mwenyekiti wa Taifa wa NCCR-Mageuzi
na amesoma fani ya uhandisi wa majengo.

No comments:
Post a Comment