Friday, 14 March 2014

MAONI: Serikali isiwasujudie waandishi wa nje

Jumanne iliyopita tulichapisha habari kuhusu ujio wa mwandishi wa Gazeti la Daily Mail la Uingereza, Martin Fletcher, ambaye aliandika habari katika toleo la gazeti hilo la Februari 9, mwaka huu kwamba Serikali ya Tanzania imeshindwa kukomesha mauaji ya tembo na faru ambao wako katika hatari ya kutoweka, akiwatuhumu baadhi ya maofisa wa Serikali na jamaa wa Rais kuwa sehemu ya mtandao mkubwa wa ujangili.
Ujio huo umewashangaza wengi, kwani pamoja na Serikali kukanusha kumwalika, mwandishi huyo amesema ziara yake nchini imetokana na mwaliko wa Serikali. Hata hivyo, sisi hatuoni kama kualikwa ama kutoalikwa na Serikali ni jambo linalostahili kujadiliwa kwa kuwa sera ya uhariri ya magazeti yenye hadhi kama Daily Mail inawaelekeza na kuwasisitizia waandishi kufuata maadili ya taaluma yao, ambayo ni kuandika ukweli hata kama ukweli huo utawauma watu waliowafadhili ama kuwawezesha kupata habari.
Hivyo, hatutazamii mwandishi Fletcher apindishe habari au aandike habari za kuifurahisha Serikali kwa sababu tu ya kufadhiliwa na kuruhusiwa kuingia katika sehemu nyeti ambazo hata waandishi wazawa na wazalendo wa hapa nchini hawaruhusiwi. Kwa kuzingatia utamaduni, maadili na weledi wa waandishi hao, utakuwa muujiza kama mwandishi huyo atakubali ‘kununuliwa’ au kufadhiliwa na Serikali ili taarifa atakazotoa baada ya ziara yake nchini ziisafishe kutokana na taarifa za awali kwamba haifanyi juhudi za kutosha kuwalinda wanyamapori.
Imeripotiwa kuwa mwandishi huyo pamoja na mpigapicha wake wamepewa mapokezi mazuri nchini na kuingizwa katika maeneo nyeti kama ghala za kuhifadhia shehena za meno ya tembo yanayokamatwa, huku wakiwaacha maofisa katika Wizara ya Maliasili na Utalii wakiwa vinywa wazi. Pia waliruhusiwa kupiga picha kinyume na utaratibu na baadaye wakapelekwa Hifadhi ya Selous kwa ndege ya Idara ya Wanyamapori.
Wizara ya Maliasili na Utalii imekiri kuwa ziara ya mwandishi huyo imetokana na uamuzi wake wa kuweka uwazi suala hilo na kwamba waandishi wengine wa BBC na CNN wameomba kufanya ziara kama hiyo.
Ni wazi kuwa uamuzi huo ni jitihada za  kujikwamua na lawama za serikali kushindwa kukomesha vitendo vya ujangili na ndio maana Rais Kikwete alikwenda katika vituo vya utangazaji vya BBC na CNN, wakati waziri husika alikutana na wahariri wa magazeti ya Daily Mail na Mail on Sunday kufafannua suala hilo.
Tumezungumzia ziara ya wageni hao kwa kirefu ili kuonyesha jinsi Serikali inavyowatetemekea waandishi wa nje na kuwapuuza wa ndani, kiasi cha  kutotaka kwa makusudi kutoa habari kwa waandishi wa ndani au kukutana nao kuzungumzia masuala muhimu ya nchi.
Tulitarajia viongozi wa juu wa serikali wangekutana na vyombo vya habari vya ndani na kutoa ufafanuzi wa kina wa suala hilo ili wananchi wapate picha halisi ya nini kilitokea kabla ya kwenda nalo kwa waandishi wa nje.
Lakini juhudi kubwa ilielekezwa katika kutoa ufafanuzi na ushirikiano kwa vyombo vya habari vya nje, akiwemo mwandishi huyo wa Uingereza. Vyombo vya habari vya ndani vitasaidia serikali pale tu itakapoamua kuwa ya uwazi na kutoa ushirikiano kwa waandishi hasa katika masuala muhimu na nyeti yanayohusu mustakabali wa  taifa hili. Serikali inajidhalilisha kwa kudhani inawajibika kwa nchi zinazotoa misaada badala ya wapigakura waliowapa uhalali wa kukaa madarakani.

No comments: