Wednesday, 20 November 2013

Viongozi AU wamejidhalilisha kesi ya ICC

Baada ya wakuu wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU), kutumia mabilioni ya fedha za walipakodi wa nchi zao kufanya kampeni ulimwengu mzima kwa lengo la kuwanusuru Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya na makamu wake, William Ruto wasishtakiwe katika Mahakama ya Uhalifu (ICC), hatua ya Baraza la Usalama kulikataa Azimio hilo wiki iliyopita bila shaka itakuwa imeufedhehesha na kuufadhaisha Umoja huo mbele ya jumuiya ya kimataifa.
Rais Kenyatta, Ruto na mtangazaji Joshua arap Sang walifunguliwa mashtaka ICC kwa kuhusishwa na vurugu zilizotokea Kenya baada ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2007, ambapo zaidi ya watu 1,500 walipoteza maisha, huku maelfu wakiachwa bila makazi. Katika hatua ya kushangaza, viongozi hao wa AU waliamua kuinunua kesi hiyo kwa kutishia kwamba wangezitoa nchi zao katika Mkataba wa Roma ulioanzisha ICC iwapo mashtaka hayo yasingefutwa.
Baada ya mkakati huo kukwama walikuja na kitu kipya. Kwamba ICC imekuwa na sera za kibaguzi dhidi ya viongozi weusi barani Afrika na kusema ndiyo maana inawalenga viongozi hao pekee. Lengo lilikuwa kuwachochea raia wa nchi zao barani Afrika waione ICC kama chombo cha kikoloni na chenye ubaguzi dhidi yao na viongozi wao, hivyo wazishinikize serikali zao kujitoa uanachama wa Mahakama hiyo. Viongozi hao walitegemea raia wa nchi zao wafanye maandamano na kuilaani ICC na mataifa yote yanayoiunga mkono.
Kinyume chake, vyombo vya habari na asasi za kiraia barani humo viliwaelimisha na kuwahamasisha wananchi ili watambue njama za viongozi wa nchi zao zenye lengo la kuitenga ICC ili kuendeleza ubabe na utawala wa mabavu, ukandamizaji, uvunjaji wa haki za binadamu na mauaji ya raia wasio na hatia.
Hata hivyo, hata baada ya njama hizo kugundulika, viongozi hao kupitia AU walibadili mbinu na kuitaka ICC ihamishie kesi hiyo barani Afrika, hasa nchini Kenya au Tanzania kwa maelezo kwamba Afrika ina uwezo wa kujiamulia mambo yake yenyewe. Mbinu hiyo pia ilishindwa, kwani ICC iligundua kwamba Afrika haina mfumo wa kimahakama ulio imara wa kuwawajibisha viongozi wa nchi wanaokiuka haki za binadamu.
Pamoja na AU kuwachochea washtakiwa wasihudhurie kesi zao ICC, wao walisema watahudhuria, pengine kwa kutambua athari na madhara ya kutokufanya hivyo. Ruto tayari amehudhuria kesi yake na Rais Kenyatta atafanya hivyo Februari 2014. Hapo ndipo AU ilipolazimika kutupa karata ya mwisho kwa kuandaa Azimio na kuliwasilisha katika Baraza la Usalama la UN, ikitaka kesi za kina Kenyatta ziahirishwe kwa mwaka mmoja ili viongozi hao wakabiliane na tishio la usalama nchini Kenya kutokana na tukio la kigaidi lililotokea jijini Nairobi hivi karibuni.
Hata hivyo, mbinu hiyo pia imeshindwa, baada ya Baraza la Usalama kulikataa Azimio hilo wiki iliyopita. Ni aibu iliyoje kwa viongozi wa Afrika kuwakingia kifua watawala wenzao, pasipo kujali waathirika wa ghasia za mwaka 2007, ambao wamesubiri kwa muda mrefu kupata haki zao pasipo mafanikio. Sisi tunasema uamuzi wa Baraza la Usalama ni ushindi kwa wana wa Afrika, wakiwamo wananchi wa Kenya ambao theluthi mbili walisema kupitia kura ya maoni wiki iliyopita kwamba kesi dhidi ya Rais Kenyatta na wenzake ziendelee kusikilizwa ICC.

No comments: