Dar es Salaam. Mwaka 2007 baada
ya aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa kujiuzulu na nafasi yake,
Mizengo Pinda aliyeshika nafasi yake alitarajiwa kuja na moto mkali
zaidi.
Itakumbukwa kuwa Lowassa aliyeangushwa na kashfa
ya mradi tata wa umeme wa Richmond, alishaanza kuonyesha machachari yake
hasa katika suala la elimu ambapo alihamasisha ujenzi wa shule za
sekondari za kata na miradi mingine.
Pinda aliingia akiwa amevaa ngozi ya kondoo, huku
akijiita mtoto wa mkulima. Leo ni miaka sita imepita, tunamwona Pinda
halisi alivyo. Kuna kila dalili kwamba amepwaya katika nafasi hiyo.
Tofauti na walivyokuwa mawaziri wakuu wengine,
Pinda hajaonyesha ubunifu katika mambo na kuyasimamia. Badala yake
amekuwa mtu wa kuonekana wakati wa matukio.
Kukitokea vurugu, wananchi wa Mtwara wameandamana,
Waziri Mkuu Pinda anakwenda kutuliza, madaktari wamegoma, anakwenda
kuzungumza nao, wenye malori na mabasi wamegoma, anakwenda
kuwabembeleza.
Huu ni udhaifu, haiwezekani kiongozi ashughulikie
matukio tu wakati anaweza kuboresha utendaji ili mambo yasiharibike.
Kutokana na udhaifu huo, hata mawaziri walio chini yake hawawajibiki
ipasavyo. Ndiyo maana hivi karibuni, Wabunge wanaoendelea na kikao mjini
Dodoma walimtaja kuwa mmoja kati ya mawaziri wanaopaswa kuwajibika
kutokana na kushindwa kusimamia kazi zao.
Wabunge hao waliomba kujadili kwa dharura
utekelezaji wa Operesheni Kimbunga na Operesheni Tokomeza, huku wengi
wakiwataja wazi mawaziri kadhaa akiwemo yeye Pinda, Dk Emmanuel Nchimbi
(Mambo ya Ndani), Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii), David Mathayo
David (Mifugo na Uvuvi) na Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa).
Pinda analalamikiwa kwa kauli yake aliyoitoa
bungeni katika mkutano uliopita akivitaka vyombo vya usalama kuwapiga
wananchi wanaokiuka sheria.
Kutokana na usimamizi hafifu na kauli zake,
kumekuwa na mauaji ya wananchi wasio na hatia kwenye operesheni ya
ujangili wa meno ya tembo, kumekuwa na migogoro ya wakulima na wafugaji
isiyokwisha, hali ya elimu imekuwa mbaya na mengineyo. Inawezekana
nafasi ya uwaziri mkuu inakosa nguvu kwa sababu, Katiba inampa nafasi
rais kama mtendaji.
Baadhi ya nchi hasa za kifalme, Waziri Mkuu ndiyo
mwenye mamlaka ya mwisho, nyingine hazina cheo cha Waziri Mkuu, badala
yake anakuwepo tu makamu wa rais. Hiyo yote ni kuondoa migongano ya
madaraka kwa sababu huwezi kuwa na rais mtendaji na waziri mkuu mtendaji
kwa wakati mmoja, ni lazima mmoja atakuwa mtumwa wa mwenzake.
Hata hivyo, bado Pinda angeweza kutumia mamlaka
aliyonayo kujijengea heshima kwa Taifa kiutendaji kama walivyofanya
mawaziri wakuu wengine.

No comments:
Post a Comment