Monday, 8 April 2013

Uhuru! Uhuru! Kesho ‘hakunaga’ Kenya


















Kesho kuapishwa akiwa ameshikiwa biblia na mke wake kama ilivyokuwa kwa Obama
Nderemo ,shamra shamra ,na vifijo za kuapishwa kwa Rais wa awamu vya nne nchini Kenya  zitasikika kesho katika Uwanja wa mpira wa Arap Moi.
Kesho Rais mteule wa Kenya,  Uhuru Kenyatta anatarajiwa kuapishwa baada ya kushinda uchaguzi mkuu wa nchi hiyo uliofanyika Machi 4 mwaka huu.
Uhuru anachukua nchi hiyo akiwa ni rais wa nne ambapo awali alitanguliwa na baba yake mzazi   Jomo Kenyatta aliyeongoza kuanzia mwaka 1964 mpaka 1978, kisha akafuata mzee Arap Moi  na Mwai Kibaki.
Kuapishwa kwa Rais huyo kulichelewa kutokana na kufunguliwa kwa kesi na mpinzani wake  Raila Odinga ambaye alipinga matokeo hayo kwa kubaini kulikuwa na udanganyifu.
Lakini hata hivyo pingamizi hilo halikufua dafu kwani mahakama ilimuidhinisha Kenyatta kuwa ndiye mshindi halali nchini humo.
Baada ya mahakama ya juu kutoa uamuzi huo ,kwa upande wake Raila Odinga alikubali yaishe kwa kusema kwamba alishatoa ahadi ya kukubaliana na uamuzi wa mahakama.
Uhuru alishatamka wiki iliyopita  kwamba wakati wa kuapishwa hataapa kwa kuinua Biblia bali atasaidiwa na mkewe kama alivyoapishwa Rais Obama wa Marekani.
Akidhibitisha hilo Mkuu wa Majeshi ya Kenya (KDF) Jenerali Julius Karangi alisema  kuwa Kenyatta aliomba kwamba mkewe Margaret Kenyatta amshikie Biblia atakapokuwa akiapishwa.
“Hili ni ombi la rais mteule na itakuwa vyema tukubali ombi lake katika siku hii ya kihistoria,” alisema Jenerali Karangi.
Kenyatta ataweka  tu mkono wake wa kushoto juu ya Biblia ikishikiliwa na mkewe, katika kile anachotaja hatua ya kuachana na mtindo wa awali wa kuapisha marais wa Kenya wakiinua Biblia.
Kesho  Rais Mwai Kibaki atamkabidhi katiba Mpya Kenyatta, ambayo ilianza kutumika mnamo Agosti 2010. Mtindo huu utakuwa wa kwanza tangu nchi hiyo kupata Uhuru.
Sherehe hiyo itafanyika katika Uwanja wa Michezo wa Moi Kasarani, ambapo pia Naibu wa Rais William Ruto ataapishwa.
Shughuli hiyo inatarajiwa kumalizika saa 7.45. Kamati ya Mamlaka ya Ofisi ya Rais tayari ina ratiba ya mpangilio wa shughuli hiyo.
Utaratibu uliowekwa ni kwamba  wageni watasimama  pindi Rais Kibaki anayeondoka madarakani atakaowasili, pia itapigwa  saluti na mizinga 21.
Kenyatta atapambwa kwa vifaa vya mamlaka ambavyo ni pamoja na Mkuu wa Nakshi (CGH), pia atapokea mkuki, ngao na katiba.
Zana hizo zinaashiria mamlaka; kwa mfano Katiba inasimamia Kenya na watu wake, mkuki unasimamia Amiri Jeshi Mkuu ilhali CGH ni heshima kubwa zaidi Kenya.
Mkuki huo ni ule ule uliopitishwa kutoka kwa Hayati Mzee Jomo Kenyatta hadi kwa Rais Mstaafu Daniel Moi, kisha kwa Rais Kibaki na sasa atakabishiwa  Kenyatta.

Kalonzo aaga kwa sherehe
Wakati kesho Uhuru akijiandaa kuapishwa kuwa Rais mpya wa nchi hiyo, Makamu wa Rais anayeondoka madarakani Kalonzo Musyoka aliandaa sherehe kubwa nyumbani kwake kwa lengo la kuwaaga wafanyakazi wenzake.
Wafanyakazi hao wakiongozwa na wakuu wa idara mbali mbali waliandaliwa chakula maridadi kabisa kikisindikizwa kwa hotuba  zenye kuvutia za kumsifia kiongozi huyo.
Kiongozi huyo alisifiwa  kutokana na uongozi wake bora katika wizara hiyo na akiwa msaidizi mkuu wa rais.
Kwenye hotuba yake makamu wa Rais  huyo aliyeandamana na mkewe Pauline Kalonzo, aliwapongeza wafanyakazi wote wa wizara hiyo kutokana na ushirikiano wao akisema kwamba kujitolea kwao kutoa huduma kuliiletea sifa wizara hiyo.

No comments: