Thursday, 13 March 2014

Daraja Kigamboni neema au balaa?

Pembezoni mwa Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Tanzania (Tec), ujenzi unaendelea wa barabara na daraja la kuunganisha Mji wa Kigamboni na Jiji la Dar es Salaam, eneo la Mkondo wa Kurasini. Ujenzi huo unafanywa na kampuni mbili kutoka nchini China.
Kampuni hizo ni; China Railway Jiangchang (T) Ltd na China Major Bridge, mradi ambao unatarajiwa kukamilika Januari 2015 ukigharimu dola 136 milioni za Marekani, fedha ambazo asilimia 60 zinatolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na kiwango kingine kinalipwa na serikali.
Ujenzi huo unafanyika ikiwa ni sehemu ya kuwaondolea kero ya Kivuko wakazi wapatao 679,291 sawa na asilimia 5.7 ya watu wote wa Dar es Salaam na idadi hiyo ni tofauti na mamia wengine ambao wanaenda eneo hilo kila siku kwa ajili ya shughuli tofauti zikiwamo za kiuchumi.
Eneo la Kigamboni ambalo limelengwa kuwa mji mpya wa kisasa, lina utajiri mkubwa wa mazao mbalimbali ya chakula, biashara kama vile mbogamboga, matunda, viazi vitamu, magimbi, nazi, korosho na mazao ya baharini wakiwamo samaki, mapambo ya majumbani na bidhaa nyingine.
Pia mji huo una hifadhi historia kwani maeneo ya Mbwamaji, Puna, Kimbiji, Pembamnazi, Buyuni na kwingineko kuna mabaki ya majengo ya kihistoria ambayo hata hivyo yanatoweka kutokana na utunzaji na harakati za ujenzi wa nyumba za kisasa.
Pia eneo hilo linasifika kwa kuwa na fukwe zenye mchanga wa kuvutia na mandhari nzuri za kupendeza hali ambayo inachangia kuwavutia watalii na wageni wengine wanaotembelea eneo hilo ambalo pia upande mwingine ina hazina kubwa ya jiwe la jasi ambalo hutumika kutengenezea saruji.
Kulingana na mkandarasi ambaye ni mbunifu wa mradi huo ambalo ni la kuning’inia (Cable-Stayed Bridge), lina urefu wa mita 680 na upana wa mita 27.5 na linatarajiwa kuwa mbadala wa Kivuko cha Kigamboni ambacho kina pantoni za Mv Kigamboni na Magogoni.
Ujenzi huo unakaribia kukamilika, lakini hadi sasa gharama za kulitumia daraja hilo kwa wananchi wa kawaida, wenye magari, baiskeli, mikokoteni na vyombo vingine bado hazijainishwa. Suala hilo linawaacha watu weni katika maswali mengi kuliko majibu.
Ingawa hakijatajwa kiwango kitakachokuwa kinatozwa kama ada na ushuru mwingine, lakini bado kuna utata iwapo mradi huo utakamilika kwa wakati kutokana na sababu nyingi ikiwa ni pamoja na ukweli kuwa mradi umefikia zaidi ya asilimia 50 ya ujenzi wake, lakini kuna utata iwapo ujenzi utakamilika kwa wakati.
Hali hiyo inatokana na ukweli kuwa hadi hivi sasa serikali haijatoa kiasi chochote kati ya asilimia 40 ya fedha ambazo wanatakiwa kuchangia ili kukamilisha mradi huo hali ambayo inadaiwa kukwamisha upatikanaji wa fedha za fidia kwa baadhi ya watu ambao wanaguswa na mradi.
Msimamizi wa mradi huo, Mhandisi Karimu Mataka wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), anakiri serikali kutokutoa fedha ambazo iliahidi hadi sasa, na hali hiyo imechangia mradi kushindwa kukamilika Januari mwakani kama ilivyokadirwa na badala yake sasa unatarajiwa kukamilika Juni mwakani.
John Ngoma maarufu kwa jina la Jitu,mkazi wa eneo la Kijibweni ambaye eneo lake limechukuliwa kwa ajili ya kutoa nafasi ya utekelezaji wa mradi huo anasema ni vizuri wakaelezwa kiasi cha fidia watakachopewa kabla ya uthamini kufanywa jambo ambalo linapingwa na mfumo mzima wa fidia.
Kulingana na taratibu na kanuni za fidia, zinafanyika kwanza, kisha ndio malipo hupangwa tofauti na wanavyotaka wakazi hao ambao wanataka waambiwe kwanza watalipwa nini.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Injinia Mussa Iyombe, alipotembelea kujionea maendeleo ya ujenzi wa daraja hilo, anasema lilitarajiwa kukamilika Januari mwaka 2015, lakini sasa itaenda hadi Juni na wakazi wa eneo hilo ambao anasema idadi yao haizidi watu wanne suala lao limefikishwa wizarani.
Anasema ujenzi wa daraja hilo ulitarajiwa kukamilika Januari mwakani, lakini kutokana na changamoto walizokutana nazo wahandisi chini ya bahari na kwa wananchi zimewafanya wachelewe na sasa wanatarajia kukamilisha kazi hiyo Julai mwakani.
Mhandishi anasema kuwa licha ya changamoto zote wakandarasi wamekuwa wakiendelea vizuri na kile ambacho kimefanyika hadi hivi sasa kinatoa matumaini kwa Watanzania kuwa mradi utakamilika kwa wakati hivyo kuwaondolea kero.
Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Vijibweni, Bahari Mohamed anasema kimsingi fedha za fidia kwa ajili ya watu hao ambao wamegoma kutoa nafasi kwa mradi zipo na iwapo wataridhia na kuvunja nyumba zao watalipwa na iwapo wataendelea na mgomo huenda nyumba hizo zikavunjwa kwa nguvu na fidia wataifuata wakitaka.
“Fedha zipo isipokuwa wamegoma watu watatu katika eneo ambako wamejenga nyumba, mmoja wao anamiliki kiwanja ambacho hakijaendelezwa,” anasema Mohamed.
Mohamed anasema daraja litakuwa na faida kiuchumi iwapo wakazi wake watalitumia vizuri na kuwekwa utaratibu wa kueleweka.
Anasema ingawa hajui watu watatozwa kiasi gani cha fedha wakati wa kuvuka, amedokezwa kwamba waenda kwa miguu watapita bure isipokuwa wale wenye vyombo vya usafiri kama vile pikipiki, magari na mikokoteni.
“Nasikia waenda kwa miguu itakuwa bure hilo halina uhakika kwani hadi sasa haijaelezwa gharama zake zitakuwa vipi,” anasema.
Mmoja wa wachukuzi wa abiria katika boti iitwayo Kilimanjaro katika eneo hilo, Idrissa Hussein anasema wao wataangalia upepo unavyoeenda kwani wamekuwa wakitoa huduma hiyo kwa kipindi kirefu tena katika mazingira magumu.
“Kama watatoza fedha watu kuvuka tutaangalia ni kiasi gani kama italipa tutaendelea na huduma kwa kiwango cha sasa au pungufu yake la sivyo tutaangalia jambo lingine la kufanya kwani mashine na vyombo bado ni mali yetu,” anasema.
Mkazi wa eneo hilo, Jonathan Ngosha anasema endapo daraja hilo litatumika kutoa huduma kwa wananchi, litakuwa ni msaada mkubwa kwao.
Lakini anasema Daraja la Kigamboni likitumiwa kama kitegauchumi, watu wengi wataendelea kutumia boti kuvuka kutoka Kigamboni hadi upande wa pili wa maeneo ya Kurasini.
Mkazi huyo anataka gharama za matumizi ya daraja hilo ziwe wazi kwa ajili ya kuwaandaa wakazi wa eneo hilo na sio kuwa kimya kama ilivyo sasa kwani hali hiyo inazua maswali mengi kuliko majibu.

No comments: